Sura 3

1 Kwa kumaliza, wandugu zangu, mufurahi kwa ajili ya kuungana kwenu na Bwana. Hainiuzi kitu kuwaandikia tena maneno yale yale niliyowaandikia mbele. Hayo yote ni kwa ajili ya kuwakingia hatari. 2 Mufanye angalisho na watenda maovu, wale imbwa wanaotia mukazo juu ya kushika tu desturi ya kutahiriwa. 3 Sisi ndio wenye kutahiriwa kwa kweli, maana tunamwabudu Mungu kwa uongozi wa Roho wake na kujivuna kwa ajili ya Yesu Kristo. Sisi hatuweki tumaini letu katika mambo ya kimwili. 4 Lakini mimi vilevile niko na haki ya kuweka tumaini katika mambo ya kimwili. Kama kuna mtu anayejizania kuwa na sababu ya kutumainia mambo ya kimwili, mimi ninamupita. 5 Nilitahiriwa nilipokuwa na umri wa siku nane. Mimi ni Mwisraeli, wa kabila la Benjamina, Mwebrania wa asili kabisa. Kuelekea mambo ya Sheria ya Kiyuda, nilikuwa Mufarisayo, 6 nilikuwa na bidii sana hata nilitesa kanisa. Kuelekea mambo ya kuhesabiwa kwa njia ya kushika Sheria, mimi sikupatikana na kosa lolote. 7 Lakini mambo yote yaliyokuwa ya faida kwangu, sasa kwa ajili ya Kristo, ninayahesabu kama kihombo. 8 8 Bila shaka, ninahesabu mambo yote kuwa kihombo kwa ajili ya faida kubwa ya kujua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa ajili yake nimekubali kupoteza vyote, nikivihesabu kuwa kama mavi, kusudi nimupate Kristo 9 na kuungana naye kabisa. Nami sihesabiwi haki tena kufuatana na mambo niliyofanya, ndiyo ile haki inayopatikana kwa njia ya kushika Sheria. Lakini ninahesabiwa haki kwa njia ya kumwamini Kristo, ndiyo ile haki inatoka kwa Mungu, naye anamuhesabia haki yule anayeamini. 10 Kitu ninachotaka tu, ni kumujua Kristo na uwezo wa ufufuko wake na kushirikiana naye katika mateso yake, nako kufa kwangu kufanane na kufa kwake. 11 Nipate hivi tumaini kwamba nitafufuka vilevile. 12 Sitaki kusema kwamba nimekwisha kufikia mwisho au kwamba nimekwisha kuwa mukamilifu. Lakini ninakaza mwendo kusudi nipate kushinda na kupokea zawadi, kwa maana Yesu Kristo amekwisha kunipokea nikuwe wake. 13 Wandugu zangu, sihesabu kwamba nimekwisha kupokea zawadi, lakini ninafanya jambo moja tu: ninasahau yanayokuwa nyuma, nikifukuzia yanayokuwa mbele yangu. 14 Kwa hiyo ninakaza mwendo mpaka mwisho nipate kupokea ile zawadi Mungu aliyotuitia katika mbingu kwa njia ya Yesu Kristo. 15 Sisi wote tunaokomaa kiroho, tukuwe na shabaha hiyo moja. Na kukiwa wamoja katikati yenu wanaokuwa na mafikiri mbalimbali, Mungu atawafunulia maneno yale. 16 Ingawa hayo yote, basi tuendelee mbele tokea kwenye hatua ile tumekwisha kufikia. 17 Wandugu zangu, mufuate mufano wangu, muwaangalie vizuri wale wanaofuata mwenendo muliouona kwetu. 18 Mimi nimewaambia mara nyingi, nami ninawaambia tena kwa machozi: kuna watu wengi wanaoonyesha kwa njia ya mwenendo wao kwamba kufa kwa Kristo juu ya musalaba ni chukizo kwao. 19 Mwisho wao ni uharibifu, sababu mungu wao ni kushibisha tumbo zao. Wanajivuna kwa kufanya mambo ya kuwafezehesha. Nayo mafikiri yao ni juu ya vitu vya dunia hii. 20 Lakini sisi ni wenyeji wa mbingu, tunamungojea Mwokozi wetu Bwana Yesu Kristo, afike kutoka kule. 21 Yeye atabadilisha huu mwili wetu wa uzaifu na kuufananisha na mwili wake wa utukufu kwa nguvu ambayo kwa njia yake anaweza kuwa na mamlaka juu ya vitu vyote.