Sura 4

1 Kwa hiyo wandugu zangu wapendwa, niko na hamu sana ya kuwaona tena. Ninyi ndio munaokuwa furaha yangu na zawadi ya ushindi nitakayopokea. Ninyi wapendwa wangu, ninawaomba musimame imara katika ushirika wenu na Bwana. 2 Ninakusihi wewe Ewodia na wewe Sintike, muishi katika masikilizano mbele ya Bwana. 3 Na wewe vilevile mtumishi mwenzangu mwaminifu, ninakuomba uwasaidie wanawake hao, kwa maana walisumbuka sana pamoja nami katika kazi ya kutangaza Habari Njema. Kuko vilevile Klementi na wenzangu wengine wa kazi. 4 Mufurahi siku zote katika kuungana kwenu na Bwana. Na tena ninasema: Mufurahi! 5 Muonyeshe upole wenu kwa watu wote, kwa maana Bwana yuko karibu kurudia. 6 Musijisumbue juu ya neno lolote, lakini katika kila neno mutoe mahitaji yenu kwa Mungu, mukimwomba, mukimusihi na kumushukuru. 7 Na amani ya Mungu inayopita ufahamu wa mtu yeyote, italinda mioyo yenu na nia zenu salama katika kuungana kwenu na Yesu Kristo. 8 Kwa kumaliza, wandugu zangu, muweke mafikiri yenu juu ya mambo yote yanayokuwa ya kweli, ya heshima, ya haki, safi, ya kupendeza, nayo mambo yote yanayostahili sifa na ya utu wema. 9 Mushike mambo yote muliyojifunza na kupokea toka kwangu, nayo yote muliyosikia na kuona kwangu. Naye Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi. 10 Nilipata furaha kubwa katika kuungana na Bwana kwa kuona munakumbuka tena kunisaidia. Sitaki kusema kwamba mulinisahau, lakini hamukupata wakati wa kuonyesha kwamba munanishugulikia. 11 Na sisemi hivi kwa sababu ninakosewa na kitu, kwa maana ninajizoeza kufurahi na kile ninachokuwa nacho. 12 Ninajua kuishi katika ukosefu na ninajua kuishi katika utajiri. Nimejizoeza kufurahi fasi zote na katika kila hali: ikiwa hali ya kuwa na vyakula kwa uwingi au ya njaa, ikiwa hali ya utajiri au ya ukosefu. 13 Ninaweza vyote kwa njia ya Kristo anayenitia nguvu. 14 Lakini, mumefanya vizuri kwa kushirikiana pamoja nami katika taabu yangu. 15 Ninyi Wafilipi munajua vizuri wenyewe kwamba nilipotoka Makedonia, tangu mwanzo wa kuhubiri Habari Njema, ni ninyi tu ndilo kanisa moja lililoshirikiana nami katika mambo ya utoaji na upokeaji. 16 Hata wakati wote nilipokuwa Tesalonika, mulinitumia musaada mara nyingi juu ya mahitaji yangu. 17 Sitaki kusema kwamba ninatafuta tu kupokea zawadi, lakini ninataka faida iongezwe kwa upande wenu. 18 Kweli nina vitu vyote vya lazima na zaidi kupita. Sasa kwa kuwa Epafrodito ameniletea zawadi zenu zote, ninatosheka. Zawadi hizi ni kama sadaka ya ubani yenye harufu nzuri, na kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto inayokubaliwa na Mungu na kumupendeza. 19 Basi, kwa njia ya Yesu Kristo, Mungu wangu atatimiza mahitaji yenu yote kufuatana na uwingi na utukufu wa utajiri wake. 20 Mungu Baba yetu atukuzwe kwa milele na milele. Amina. 21 Musalimie watu wote wa Mungu wanaomwamini Yesu Kristo. Wandugu wanaokuwa pamoja nami wanawasalimia. 22 Watu wote wa Mungu, na hasa zaidi wale wanaokuwa katika nyumba ya Mfalme, wanawasalimia vilevile. 23 Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo iwe na mioyo yenu.