Sura 6

1 Mujiangalie musifanye matendo mema mbele ya watu kusudi mujionyeshe kwao. Kwa maana mukifanya hivi hamutapata faida kutoka kwa Baba yenu anayekuwa mbinguni. 2 Basi wakati unapomusaidia masikini, usipige baragumu, kama vile wanafiki wanavyofanya katika nyumba za kuabudia na katika barabara kusudi wasifiwe na watu. Kweli ninawaambia: wamekwisha kupata faida yao. 3 Lakini wewe, unapomusaidia masikini, ufanye tendo lile kwa uficho hata rafiki yako wa kweli asijue. 4 Hivi tendo lile halitatoka inje, naye Baba yako anayeona tendo unalofanya kwa siri, atakulipa 5 Munapoomba, musikuwe kama wanafiki, kwa maana wanapenda kuomba wakisimama katika nyumba za kuabudia na pembeni ya barabara, kusudi wapate kujionyesha mbele ya watu. Kweli ninawaambia: wamekwisha kupata faida yao. 6 Lakini wewe, unapoomba, ingia ndani ya chumba chako, funga mulango na uombe kwa Baba yako asiyeonekana. Na Baba yako anayeona tendo unalofanya kwa siri, atakulipa. 7 Tena munapoomba, musitumie maneno mengi yasiokuwa na maana kama vile wapagani wanavyofanya, kwa sababu wanawaza kama Mungu atawasikia kama wakisema maneno mengi. 8 Basi musifanye kama wao, musifanane nao kwa maana Baba yenu anajua vitu munavyohitaji mbele hamujamwomba. 9 Basi muangalie namna munavyopaswa kusema munapoomba: Baba yetu unayekuwa mbinguni, Jina lako litukuzwe; 10 Ufalme wako ukuje; mapenzi yako yafanyike katika dunia kama inavyokuwa mbinguni. 11 Utupe chakula chetu cha kila siku. 12 Utusamehe makosa yetu, kama sisi tunavyowasamehe wanaotukosea, 13 Usituache kuanguka katika majaribu, lakini utuokoe na yule Mwovu. [Kwa maana ufalme, uwezo na utukufu ni vyako hata milele. Amina.] 14 Hivi, mukiwasamehe watu wengine makosa wanayowatendea, Baba yenu anayekuwa mbinguni atawasamehe vilevile. 15 Lakini kama musipowasamehe wengine wanaowakosea, Baba yenu hatawasamehe makosa yenu vilevile. Mafundisho juu ya kufunga kula chakula 16 Munapofunga kula chakula, musifanye kama wanafiki, wanaojigeuza kuwa wenye sikitiko na kukunja nyuso zao, kusudi watu waone kwamba wanafunga. Kweli ninawaambia: wamekwisha kupata faida yao. 17 Lakini wewe unapofunga kula chakula, unawe uso wako na kuchanua nywele zako, 18 kusudi usijionyeshe kwa watu kwamba unafunga. Jambo hilo litajulikana tu kwa Baba yako anayekuwa kwa siri. Naye Baba yako anayeona tendo unalofanya kwa siri, atakulipa. Akiba ya dunia na ya mbinguni 19 Musijiwekee akiba katika dunia hii, pahali nondo na kutu vinapoharibu, nao wizi wanapotoboa nyumba na kuiba. 20 Lakini mujiwekee akiba katika mbingu, pahali nondo wala kutu visipoweza kuharibu, nao wizi wasipoweza kutoboa na kuiba. 21 Kwa maana pahali akiba yako inapokuwa, ni pale roho yako inapokuwa vilevile. Mwangaza wa mwili 22 Macho ni taa ya mwili. Kama macho yako yakiwa mazima, mwili wako wote utabaki katika mwangaza. 23 Lakini kama macho yako yanaharibika, mwili wako wote utabaki katika giza. Basi ikiwa mwangaza unaokuwa ndani yako umegeuka kuwa giza, giza hilo ni nzito sana! 24 Hakuna mtu anayeweza kuwatumikia wabwana wawili. Kwa maana atamuchukia mmoja na kumupenda mwingine; au atashikamana na mmoja na kumuzarau mwingine. Hamuwezi kutumikia Mungu na kutumikia mali vilevile. 25 Ni kwa sababu hii ninawaambia ninyi: musijisumbue kwa ajili ya maisha yenu, kwa ajili ya chakula au kwa ajili ya kinywaji, wala musijisumbue kwa ajili ya miili yenu kwamba mutavaa nini. Uzima ni wa lazima kuliko vyakula, nao mwili ni wa lazima kuliko nguo. 26 Muangalie ndege wanaoruka katika anga: wao hawapandi mbegu wala hawavuni, wala hawaweki mavuno ndani ya gala, lakini Baba yenu anayekuwa mbinguni anawakulisha! Basi ninyi si wa lazima zaidi kuliko ndege wale? 27 Nani kati yenu, kwa ajili ya kujisumbua kwake, anaweza kujiongezea hata siku moja kupita muda wa maisha yake? 28 Kwa sababu gani munajisumbua kwa ajili ya nguo? Muangalie maua jinsi yanavyoota. Hayatumiki wala kujisukia nguo. 29 Lakini ninawaambia kwamba hata mfalme Solomono katika utukufu wote aliokuwa nao hakuvaa nguo inayoweza kulinganishwa na uzuri wa moja la maua yale. 30 Basi ikiwa Mungu anavalisha majani kama hivi, yanayoonekana leo na kesho yanatoweka na kutupwa katika moto, hatawavalisha ninyi vizuri zaidi, ninyi wenye imani ndogo? 31 Basi musijisumbue kwa ajili ya chakula, kwa ajili ya kinywaji au kwa ajili ya nguo. 32 Ni wapagani ndio wanaoshugulika kwa kutafuta vitu vile vyote. Baba yenu anayekuwa mbinguni anajua kama munahitaji vitu vile vyote. 33 Lakini ninyi mushugulikie kwanza Ufalme wa Mungu na kufuata haki mbele yake, naye atawaongezea vitu vile vyote. 34 Basi musijisumbue kwa ajili ya kesho, kwa maana kesho itajisumbukia yenyewe. Kila siku ina masumbuko yake inayoitoshelea