Sura 1

1 Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Timoteo. Mimi ambaye kwa mapenzi ya Mungu, niliitwa kuwa mutume wa Kristo Yesu. Tunawaandikia kanisa la Mungu linalokuwa Korinto na watu wake wote wanaokuwa katika jimbo lote la Akaya. 2 Tunawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. 3 Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba mwenye kujaa huruma na Mungu anayefariji katika mambo yote! 4 Yeye anatufariji katika taabu yetu yote, kusudi tupate kuwafariji wale wanaokuwa katika taabu yoyote kwa kuwaletea faraja tuliyopokea kutoka kwa Mungu. 5 Basi, kwa kadiri tunavyoshiriki katika mateso mengi ya Kristo, ni kwa kadiri ile sisi vilevile tunafarijiwa sana kwa njia ya Kristo. 6 Kama sisi tunapata taabu ni kusudi mupate kufarijiwa na kuokolewa. Kama tunafarijiwa ninyi vilevile munafarijiwa na kupata nguvu ya kuwawezesha kuvumilia taabu ile ile tunayopata. 7 Kwa hivi, hatuwezi kukata tumaini tunalokuwa nalo kwenu, kwa maana tunajua kwamba kwa kuwa munashiriki katika taabu yetu, munashiriki vilevile katika kufarijiwa kwetu. 8 Wandugu, tunataka mujue taabu tuliyopata katika jimbo la Azia. Taabu ile ilitulemea sana hata tukakata tumaini lote la kuendelea kuishi. 9 Tulikuwa tumefikiri kwamba tulihukumiwa kufa. Basi, ilitokea hivi kusudi tusijitegemee sisi wenyewe, lakini tumutegemee Mungu tu anayefufua wafu. 10 Yeye ndiye aliyetuopoa toka hatari kubwa sana ya kufa, naye atatuopoa tena. Nasi tunamutumainia kwamba ataendelea kutuopoa, 11 nanyi wenyewe mutatusaidia kwa njia ya maombi. Kwa hivi Mungu atajibu kwa maombi yaliyotolewa na watu wengi kwa ajili yetu na kututendea wema, na watu wengi watamushukuru kwa ajili yetu. 12 Jambo ambalo tunajivunia ni hili: zamiri yetu inayotuhakikishia kwamba tumeishi katika dunia na zaidi kati yenu katika uaminifu na ukweli tulivyojaliwa na Mungu. Sisi hatukuongozwa na hekima ya kimtu lakini na neema ya Mungu. 13 Basi katika barua zetu tunawaandikia tu mambo yale munayoweza kusoma na kufahamu. Ninatumaini kwamba mutafahamu mambo haya kabisa, 14 maana munayafahamu sasa kwa sehemu tu. Kwa Siku ile ya kurudi kwa Bwana wetu Yesu mutaweza kujivuna kwa ajili yetu kama vile tutakavyojivuna kwa ajili yenu. 15 Katika tumaini hili nilikusudia kufika kwenu kwanza kusudi mupate furaha mara mbili. 16 Nilikusudia kupitia kwenu kwa kwenda Makedonia, kisha ningewaona tena wakati wa kurudia, kwa hiyo mungenisaidia kwa safari yangu kwenda Yudea. 17 Basi, nilipokusudia kubadilisha mupango wangu mimi nimekuwa kama kigeugeu? Wakati ninapofanya mipango yangu, mimi ninaongozwa na mafikiri ya kimtu hata nipate kusema Ndiyo na Hapana kwa mara moja? 18 Kama vile Mungu anavyokuwa mwaminifu, hakika mambo tuliyowaambia hayakukuwa ya kusema Ndiyo na Hapana kwa mara moja. 19 Kwa maana Yesu Kristo, Mwana wa Mungu ambaye Silvano, Timoteo na mimi mwenyewe tuliyemuhubiri kwenu hakukuja kusema Ndiyo na Hapana. Lakini yeye ni Ndiyo inayotoka kwa Mungu. 20 Maana yeye ndiye anayetimiza ahadi zote za Mungu. Vilevile ni kwa njia ya Yesu Kristo tunasema Amina kwa kumutukuza Mungu. 21 Ni Mungu mwenyewe ndiye anayetuimarisha pamoja nanyi katika ushirika na Kristo, na ni yeye mwenyewe ndiye aliyetuchagua. 22 Ameweka kitambulisho juu yetu kinachohakikisha kama sisi ni watu wake na kuweka Roho Mtakatifu ndani yetu kuwa rehani ya vitu vyote anavyotuwekea. 23 Ninamutaja Mungu kuwa mushuhuda wangu, yeye anajua roho yangu! Mimi nilikusudia kutorudia tena Korinto kwa sababu ya kuwasikilia huruma. 24 Hatutafuti kuwaamuru ninyi juu ya mambo yale munayopaswa kuamini, maana munasimama imara katika imani. Lakini tunataka kutumika pamoja nanyi kusudi mupate kufurahi.