Sura 23

1 Halafu Yesu akawaambia makundi ya watu na wanafunzi wake: 2 Walimu wa Sheria na Wafarisayo wamepewa madaraka ya kueleza Sheria ya Musa. 3 Basi kwa hiyo munapaswa kuwatii na kushika maneno yote wanayowaambia; lakini musifuate matendo yao, kwa maana mambo wanayoyasema, si ndiyo wanayofanya. 4 Wanafunga mizigo mizito na kuibebesha watu wengine kwa mabega, lakini wao wenyewe hawafikiri hata kidogo juu ya namna ya kuwasaidia kuibeba. 5 Wanafanya matendo yao yote tu kusudi wajionyeshe mbele ya watu. Wanajifungia kwa paji za nyuso vibweta vipana vyenye vikaratasi vya Maandiko Matakatifu. Nao wanavaa kanzu zenye pembe ndefua 6 Wanapenda kuikaa kwenye nafasi za heshima katika karamu na katika viti vya mbele ndani ya nyumba za kuabudia. 7 Wanapenda vilevile kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi za makutano, na kuitwa Mwalimu. 8 Lakini ninyi musikubali kuitwa Mwalimu, kwa maana ninyi wote ni wandugu, nanyi muko na Mwalimu mmoja tu. 9 Vilevile hapa katika dunia musimwite mtu yeyote Baba kwa maana muko na Baba mmoja tu, anayekuwa mbinguni. 10 Musikubali kuitwa Waongozi, kwa maana muko na Mwongozi Mkubwa mmoja tu, ndiye Kristo. 11 Lakini anayekuwa mkubwa kati yenu sherti akuwe mtumishi wenu. 12 Na yeyote anayejiinua, atashushwa, lakini anayejishusha, atainuliwa. 13 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munawafungia watu wengine njia ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni. Ninyi wenyewe hamuingii mule na zaidi ya hii munawazuiza wale wanaotaka kuingia. [ 14 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munanyanganya mali za wajane na kuomba maombi marefu kwa kujionyesha. Kwa sababu hii azabu yenu itakuwa kubwa zaidi!] 15 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munasafiri kuvuka bahari na inchi mbalimbali kusudi mupate kumugeuza hata mtu mmoja tu kuwa mufuasi wenu. 16 Ole kwenu, ninyi waongozi vipofu! Ninyi munaosema kwamba mtu akiapa kwa jina la hekalu, si kitu; lakini kama akiapa akitaja zahabu inayokuwa ndani ya hekalu, anapaswa kutimiza kiapo chake. 17 Ninyi wapumbafu na vipofu! Ni nini inayokuwa kubwa zaidi, zahabu au hekalu linaloifanya zahabu ile ihesabiwe kuwa takatifu? 18 Munasema vilevile kwamba mtu akiapa akitaja mazabahu, si kitu; lakini kama akiapa akitaja sadaka inayokuwa juu yake, anapaswa kutimiza kiapo chake. 19 Ninyi vipofu! Ni nini inayokuwa kubwa zaidi, sadaka au mazabahu ndiyo inayoifanya sadaka ile ihesabiwe kuwa takatifu? 20 Katika haya yote mtu anayeapa kwa jina la mazabahu anaapa kwa jina lile na kwa majina ya vyote vinavyokuwa juu yake. 21 Vilevile anayeapa kwa jina la hekalu anaapa kwa jina lile na kwa jina la Mungu anayekuwa ndani yake. 22 Naye anayeapa kwa jina la mbingu anaapa kwa jina la kiti cha kifalme cha Mungu na kwa jina la Mungu anayeikaa juu yake. 23 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munatoa fungu moja la kumi la vijani vya kukoleza chakula, lakini mumeacha mambo makubwa yanayoamuriwa na Sheria, kama vile haki, huruma, na uaminifu. Mambo hayo ndiyo muliyopaswa kushika pasipo kuacha mengine. 24 Ninyi waongozi vipofu! Munapokunywa, munachuya imbu toka katika vinywaji vyenu, lakini munameza ngamia! 25 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Ninyi ni kama mtu anayesafisha tu inje ya kikombe na sahani, lakini ndani kumejaa vitu mulivyovipata kwa njia ya wizi na tamaa mbaya. 26 Wewe kipofu Mufarisayo! Safisha kwanza ndani ya kikombe na ya sahani, na kisha inje yake kutakuwa safi vilevile. 27 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munafanana na makaburi yaliyopakaliwa chokaa, yanayoonekana kuwa mazuri kwa inje, lakini ndani yanajaa mifupa ya wafu na uchafu wa kila namna. 28 Ni vile ninyi munavyokuwa, kwa inje munaonekana kuwa wenye haki mbele ya watu, lakini ndani yenu munajaa unafiki na uovu. 29 Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munajenga makaburi ya manabii na kupamba makaburi ya watu waliokuwa wema. 30 Nanyi munasema: «Kama sisi tungaliishi katika nyakati za babu zetu, hatungalijiunga nao katika shauri la kuwaua manabii.» 31 Hivi munajishuhudia ninyi wenyewe kuwa ninyi ni ukoo wa watu waliowaua manabii. 32 Basi mutimize hayo mambo babu zenu waliyoyaanza! 33 Ninyi kikundi cha nyoka! Namna gani mutaweza kuepuka azabu ya jehenamu? 34 Kwa sababu hiyo, nitawatumia manabii na watu wenye hekima na walimu. Mutawaua wamoja wao, mutatundika wengine juu ya misalaba, mutawapiga wengine fimbo ndani ya nyumba zenu za kuabudia na kuwafukuza mji kwa mji. 35 Na hivi mutabeba lazima ya damu iliyomwangwa katika dunia pasipo kosa, tangia kuuawa kwa Abeli aliyekuwa mukamilifu mpaka kuuawa kwa Zakaria, mwana wa Barakia, muliyemwuia kwenye hekalu katikati ya Pahali Patakatifu na mazabahu. 36 Kweli ninawaambia: watu wa kizazi hiki watabeba lazima ya mambo hayo yote. 37 Ewe Yerusalema, Ewe Yerusalema. Wewe unaua manabii na kuwatupia mawe wale ambao Mungu anakutumia. Mara nyingi nilitaka kuwakusanya wakaaji wako kama vile kuku anavyokusanya vitoto vyake chini ya mabawa yake, lakini ninyi hamukutaka! 38 Angalia, makao yenu yanaachwa ukiwa. 39 Kwa maana ninawaambia, tangia sasa hamutaniona tena mpaka mutakaposema: «Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana.»