Sura1

1 Yesu alizaliwa Betelehemu katika Yudea wakati wa utawala wa mfalme Herode. Kisha kuzaliwa kwake, watu wenye elimu kutoka mashariki wakafika Yerusalema. 2 Nao wakauliza: «Yuko wapi yule mtoto aliyezaliwa kuwa mfalme wa Wayuda? Tumeona nyota yake inayomutambulisha, nasi tumekuja kumwabudu.» 3 Mfalme Herode aliposikia maneno haya, akafazaika sana pamoja na wakaaji wote wa Yerusalema 4 Akawakusanya wakubwa wote wa makuhani na walimu wa Sheria kwa kuwauliza wapi Kristo atakapozaliwa. 5 Nao wakamujibu: Betelehemu katika Yudea, kwa maana ilisemwa hivi kwa njia ya nabii: 6 «Ewe Betelehemu, katika inchi ya Yuda, wewe si mudogo kabisa kati ya miji mikubwa ya Yuda, maana ndani yako atatoka mutawala, atakayechunga watu wangu, ndio Waisraeli.» 7 Basi Herode akawaita kwa siri wale wenye elimu kusudi wamujulishe hakika wakati gani nyota ile ilipotokea. 8 Kisha akawatuma Betelehemu, akiwaambia: «Mwende mupeleleze habari kamili za mtoto yule. Nanyi mutakapomwona munijulishe kusudi mimi vilevile niende kumwabudu.» 9 Kisha kumusikiliza mfalme, wakaondoka. Ile nyota waliyoiona tokea mashariki iliwatangulia, nayo ikaenda na kusimama juu ya pahali mtoto alipokuwa. 10 Na wakati walipoiona wakafurahi sana. 11 Wakaingia ndani ya nyumba, wakamwona mtoto pamoja na mama yake, Maria. Wakapiga magoti na kumwabudu mtoto. Kisha wakafungua mizigo yao na kumutolea zawadi ya zahabu, ubani na marasi. 12 Nyuma ya maneno haya, Mungu akawaonya katika ndoto kwamba wasirudie tena kwa Herode, kisha wakarudia katika inchi yao wakipitia njia nyingine. 13 Wale watu wenye elimu walipokwisha kwenda, malaika wa Bwana akamutokea Yosefu katika ndoto na kumwambia: «Amuka, utwae mtoto pamoja na mama yake na mukimbilie Misri. Mukae kule mpaka nitakapokuambia kwamba urudie, kwa maana Herode anamutafuta mtoto kusudi amwue.» 14 Basi Yusufu akaamuka, akamutwaa mtoto pamoja na mama yake, nao wakaondoka usiku ule kwenda Misri. 15 Akakaa kule mpaka Herode alipokwisha kufa, kusudi yatimie maneno haya Bwana aliyosema kwa njia ya nabii: «Nilimuita mwana wangu arudie toka Misri.» 16 Herode alipoona kwamba wale watu wenye elimu wamemudanganya, akakasirika sana. Akatuma watu Betelehemu na popote kandokando yake kwa kuua watoto wote waliokuwa na umri wa miaka miwili na chini yake. Alifanya vile kufuatana na jinsi alivyohakikishwa na wale wenye elimu juu ya wakati nyota ilipotokea. 17 Halafu yakatimia maneno haya yaliyosemwa kwa njia ya nabii Yeremia: 18 «Sauti inasikilika toka Rama, kilio na malalamiko mengi. Ni Rakeli anayewalilia watoto wake, naye hataki kufarijiwa, kwa maana hawako tena.» 19 Herode alipokuwa amekwisha kufa, malaika wa Bwana akamutokea Yosefu katika ndoto kule Misri. 20 Akamwambia: «Amuka, utwae mtoto pamoja na mama yake, na urudie nao katika inchi ya Israeli, kwa maana wale waliotafuta kumwua wamekwisha kufa.» 21 Basi Yosefu akaamuka, akamutwaa mtoto pamoja na mama yake na kurudia katika inchi ya Israeli. 22 Lakini aliposikia kwamba Arkelao alitawala katika jimbo la Yudea kwa pahali pa baba yake Herode, Yosefu akaogopa kwenda kule. Na alipokwisha kuonywa katika ndoto, akaenda katika jimbo la Galilaya. 23 Kule akakaa katika mji ulioitwa Nazareti, kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya manabii: «Ataitwa mtu wa Nazareti.»